Dar es Salaam. Mkuu wa wilaya ya Ilala, Sophia Mjema ameagiza manispaa ya Ilala kuwapatia tenda za uzoaji takataka katika mitaa vikundi vya wanawake kwa sababu wana uwezo mkubwa wa kufanyakazi hiyo.
Alitoa agizo hilo kutokana na kusuasua kwa uzoaji takataka na katika maeneo mengi wakandarasi hakuna.
Alitoa agizo hilo jana katika viwanda vya Mashujaa Mnazi Mmoja wakati akifunga tamasha la ‘Wajasiliamari Festival’ lililofanyika kwa siku tatu, lililoandaliwa na Guru Planet Ltd kwa kushirikiana na manispaa ya Ilala.
Mjema alipongeza vikundi 74 na wajasiliamari 856 walioshiriki katika tamasha hilo kutoka manispaa za Ubungo, Kinondoni, Temeke na Kigamboni akisema wanatekeleza agizo la Rais John Magufuli la kujenga dhana ya uchumi wa viwanda katika kuelekea uchumi wa kati.
Aliwaomba kuzingatia kauli mbinu ya maonyesho hayo kuwa ujasiliamali ni chachu ya kukuza uchumi wa nchi kwa maendeleo ya viwanda, tumia fursa zilizopo acha kulalamika.
"Natambua bado mnakabiliwa na changamoto ya mitaji na masoko lakini kuna mikakati mingi ya kuhakikisha ufumbuzi unapatikana, naomba mtoe ushirikiano kwa manispaa na wadau ili kuweza kufikia malengo," alisema Mjema.
Kwa upande wa mjasiliamari kutoka Kiwalani, Mary Raphael ambaye anajishughulisha na utengenezaji wa sababu na mafuta ya nywele ya asili, alisema wamejifunza mengi kupitia tamasha hilo lakini changamoto inayowakabili kwa sasa ni upatikanaji wa leseni ya kuwawezesha kununua kemikali ya kutengeneza sabuni na batiki.
Pia alishauri wajasiliamari wahakikishe wanapata ujuzi kutoka Sido ambapo watapatiwa cheti mbacho kitawasaidia kupata usajili na hata kwenda mahali popote kupata msaada.