Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

DC ahamasisha mazao  ya viungo vya chakula

F2748e23a1a4cb602e9991af077dfd3c DC ahamasisha mazao  ya viungo vya chakula

Wed, 9 Jun 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Ng'wilabuzu Ludigija amesema viungo mbalimbali vya chakula vinavyozalishwa nchini vinahitajika kwa kiasi kikubwa katika masoko ya ndani na nje ya nchi, hivyo wazalishaji wanatakiwa kuzalisha kwa wingi kwa kuzingatia viwango vya ubora na usalama.

Amesema wazalishaji hao wakijibidiisha na kuongeza nguvu katika uzalishaji, kutaifanya nchi kujenga uchumi endelevu wenye nguvu imara na wenye ushindani.

Alisema hayo juzi mkoani Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wajasiriamali, wachakataji, wauzaji na wasambazaji wa viungo vya vyakula kutoka mkoa huo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makala. Mafunzo hayo yaliandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

Alisema azma ya serikali ni kuhakikisha nchi inajitosheleza katika uzalishaji wa bidhaa kwa soko la ndani au nje ya nchi.

Alisema uzalishaji wa viungo unahitaji kwenda sambamba na ubora na usalama ili kulinda afya ya mlaji na kuongeza soko katika nchi za jirani.

"Uongozi wa wilaya una amini kuwa mafunzo haya ni njia mwafaka ya kuleta tija zaidi katika juhudi za kuliletea taifa letu maendeleo ya haraka kulingana na fursa zilizopo hasa kwenye sekta ya viwanda, kilimo, biashara, uvuvi na maeneo mengine," alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Upimaji wa TBS, Johanes Maganga akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Dk Yusuf Ngenya alisema mafunzo hayo yanajumuisha washiriki 100 kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo, walengwa wakiwa ni wajasiriamali ambao wanajihusisha na usindikaji, uchakataji, ufungashaji na wauzaji wa viungo vya vyakula.

Alisema kupitia mafunzo hayo washiriki wanapewa elimu juu ya majukumu ya TBS ikiwamo kanuni bora za uzalishaji, matakwa ya viwango na namna bora ya uhifadhi, ufungashaji na teknolojia ya vifungashio pamoja na taarifa za msingi zinazopaswa kuwamo kwenye vifungashio.

"Wanaelimishwa juu ya taratibu za usajili wa bidhaa za vyakula na majengo kazi ambazo hapo awali zilikuwa zikifanywa na iliyokuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA)," alisema.

Naye Meneja Mafunzo na Utafiti TBS, Hamisi Mwanasala alisema mafunzo hayo ni endelevu kwa shirika hilo, hivyo litaendelea kutoa mafunzo ya namna hiyo kwa wazalishaji, wauzaji na wasambazaji wengine wa viungo vya vyakula katika mikoa mingine kwa utaratibu.

Chanzo: www.habarileo.co.tz