Dar es Salaam. Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga leo Jumanne Novemba 19, 2019 ameshindwa kufika katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala kusikiliza rufaa aliyokata kupinga hukumu ya Mahakama ya Mwanzo Ukonga.
Katika hukumu hiyo, Odunga alitakiwa kutoa Sh7 milioni kama nusu ya gharama za matunzo aliyotumia mkewe, Medelina Mbuwuli kumsomesha mtoto wao kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha sita.
Odunga alifungua kesi kumtaliki mkewe lakini mahakama ililikataa ombi hilo, badala yake ikamtaka alipe kiasi hicho cha fedha.
Rufaa hiyo leo ilipangwa kwa ajili ya kutajwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Glory Nkwera na kutokana na mkuu huyo wa wilaya kutokuwepo mahakamani, hakimu huyo aliahirisha kuisikiliza hadi Desemba 12, 2019.
Katika maelezo ya kukata rufaa, Odunga alidai kuwa hakimu aliyesikiliza kesi yake dhidi ya Medilina alifanya kosa kutamka amlipe Sh7 milioni.
Alisema hakimu huyo alifanya kosa kwa kutokutoa talaka na kubainisha kuwa ana imani ndoa yake haipo.