Tunduru. Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Julius Mtatiro jana Alhamisi Oktoba 31, 2019 amesimamia wanafunzi watatu wa shule ya sekondari Ligoma wilayani humo kuchapwa viboko mbele ya wazazi wao.
Kabla ya kuanza kutoa maagizo ya kuchapwa viboko, alianza kuwauliza majina yao na kuwasomea makosa yanayowakabili, hasa utoro.
Hivi karibuni mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila aliwachapa viboko wanafunzi 14 wa shule ya Sekondari Kiwanja kwa madai ya kuchoma moto mabweni ya shule hiyo na kukutwa na simu.
Jana katika shule hiyo iliyopo tarafa ya Namasakata, mkuu huyo wa wilaya alimtaka mwalimu wa shule hiyo kuwachapa viboko vinne wanafunzi hao, kuagiza wapewe adhabu nyingine zisizohusiana na viboko, ikiwa ni pamoja na kuchimba visiki.
“Mwalimu Mkuu naomba umteue mwalimu atakayetoa adhabu ya viboko kwa hawa watoto halafu kesho (leo) mtawapangia adhabu nyingine.” “Mwalimu Abeli haraka nataka viboko vya nguvu, ni vingapi, vinne sio na ukigusa (mwanafunzi) tu tumeahirisha,” amesema Mtatiro.
Baada ya viboko hivyo, aliwauliza wanafunzi hao lini wataanza kwenda shule na mmoja kujibu kuwa ataripoti Jumatatu, na mkuu huyo wa Wilaya kusema wote wanapaswa kuripoti leo.