Kigoma. Mkuu wa Wilaya ya Kigoma nchini Tanzania, Samson Anga amewataka wawekezaji kuwekeza mkoani humo kwa kuwa kuna vivutio vya kila aina.
Ameeleza hayo leo Jumamosi Februari Mosi, 2020 katika uzinduzi wa wiki ya sheria.
Amebainisha kuwa kazi ya Serikali ni kuwawekea wawekezaji mazingira rafiki ili waweze kuleta maendeleo katika Mkoa huo.
"Tunawakaribisha wawekezaji kutoka ndani na nje ya Tanzania kuja Kigoma kuwekeza kwa kuwa kuna fursa mbalimbali ikiwemo Ziwa Tanganyika na zao la mchikichi na vingine vingi," amesema Anga.
Akizungumza mara baada ya uzinduzi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Ilvin Mugeta amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika mabanda ya maonyesho kuanzia leo hadi kilele cha maadhimisho hayo Februari 6, 2020, ili waweze kupata majibu ya maswali yanayowatatiza.