Dodoma. Mkuu wa wilaya ya Dodoma, Patrobas Katambi ametaja sababu za kumuweka ndani diwani wa Chang’ombe (CCM), Bakari Fundikira, akieleza kuwa inatokana na masuala ya usalama.
Katambi amesema Fundikira aliitwa polisi na kuhojiwa kwa mambo ya usalama na kisheria, kwamba alitoa agizo hilo kwa nafasi yake ya mwenyekiti wa ulinzi na usalama wa wilaya, kwamba si kwa sababu za kisiasa.
Mwishoni mwa wiki iliyopita taarifa zilisambaa kuwa diwani huyo amewekwa ndani kutokana na sababu za migogoro ya ardhi kwenye kata yake.
“Aliitwa kwa sababu ya mambo ya kiusalama, haikuwa sababu ya migogoro ya ardhi. Ni mambo ya kisheria zaidi ambayo nisingependa yaingie kwenye vyombo vya habari kuhusu sababu, lakini tambua hilo kwamba niliagiza iwe hivyo kwa nafasi yangu kama mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama,” amesema Katambi leo Jumapili Januari 13, 2019.
Hata hivyo, Katambi hakufafanua sababu hizo za kiusalama zilizosababisha diwani huyo kuwekwa ndani.