Arusha. Uongozi wa Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) umejitenga na tuhuma zinazomkabili mfanyakazi wake anayedaiwa kuomba rushwa ya ngono kwa mwanafunzi.
Taarifa iliyotolewa leo Jumanne Agosti 6, 2019 na mkuu wa kitengo cha uhusiano wa chuo hicho ,Gasto Leseiyo inaeleza kuwa taasisi hiyo ya umma inazingatia maadili na inapingana na vitendo vyote vibaya visivyoendana na utumishi wa umma.
Mtumishi huyo ambaye jina lake limehifadhiwa alikamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru) ijumaa Agosti 2, 2019 kwa mahojiano akituhumiwa kuomba rushwa ya ngono.
"Uongozi wa Chuo chetu unapenda kutoa taarifa kwa umma na wadau mbalimbali wa elimu kuwa umepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kushikiliwa kwa mtumishi wetu na Takukuru kwa tuhuma zinazomkabili," inaeleza.
Uongozi huo umeahidi kutoa ushirikiano utakaohitajika kwa vyombo vya uchunguzi wa suala hilo ili kutoa haki stahiki kwa pande zote zinazohusika .