Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Chanzo cha tembo walioua mtu, kujeruhi chabainishwa

65630 Tembo+pic

Fri, 5 Jul 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Same. Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Mkomazi mkoani Kilimanjaro Tanzania, Abel Peter, amesema tembo waliovamia maeneo ya Same na kusababisha uharibifu wa mazao na  kifo cha mtu mmoja wanatokana na  baadhi  ya wananchi kuwazingira wanyama hao  na kuanza kuwapigia honi za bodaboda jambo lililoibua hasira kwa wanyama hao.

Akizungumza na Mwananchi jana Alhamisi Julai 4, 2019, Peter alisema tembo hao ambao walikua wawili, walitoroka katika hifadhi ya Mkomazi na kuingia kwenye maeneo ya wananchi ambapo mbali ya kusababisha kifo, walimjeruhi mtu mmoja na kusababisha uharibifu wa mazao, ambayo tathimini yake haijafanyika.

Alisema kwa kushirikiana na uongozi wa wilaya hiyo kupitia kikosi cha Ujangili, wamefanikiwa kuwarudisha wanyama hao hifadhini juzi na kuwataka wananchi kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwa kuwa hali ni shwari.

“Kihistoria huwa wanyama hawa  wanakuwa na mapito yao ya kupita na huu ndio msimu wao kutokana na mazao yaliyopo mashambani kwa sasa, lakini wananchi wamelima kwenye mapito yao  na wakipita  wanawafukuza na kuwapigia kelele.”

“Hii ni hatari na ndiyo husababisha wanyama hao kukasirika na kufanya uharibifu, kwani kawaida yao huwa hawapendi kelele,” alisema Peter

Kamishna huyo alisema  tayari wamekutana na uongozi wa wilaya hiyo, kuweka mikakati ya kutoa elimu kwa wananchi ili kuchukua tahadhari pindi wanapowaona wanyama hao ili kuhakikisha hawawasogelei wala kuwapigia kelele.

Pia Soma

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Hamisi Issah, alisema tembo hao walisababisha kifo cha mtu mmoja ambaye alikuwa akichunga mazao yake yasiharibiwe na wanyama hao na kumjeruhi mtu mmoja.

Kamanda Issah alimtaja aliyefariki  ni Hansi Edes (47) mkazi wa Mheza kata ya Maore na kueleza kuwa tayari hali ya usalama imerejea katika eneo la Same baada ya tembo waliokuwa wamezagaa kurudishwa hifadhini.

Chanzo: mwananchi.co.tz