Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Chama cha wachapishaji Tanzana chataja changamoto tatu zinazokikwamisha

Wed, 28 Aug 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Chama cha Wachapishaji Tanzania (Pata) kimeeleza changamoto tatu zinazokikwamisha na kuiomba Serikali  ya Tanzania kuzifanyia kazi ili kukuza sekta ya uchapishaji nchini humo.

Moja ya changamoto hizo zilizoainishwa na mwenyekiti wa chama hicho, Gabriel Kitua ni kutokuwa na sera ya kitaifa ya vitabu inayobainisha matarajio na majukumu ya wadau mbalimbali katika mlolongo wa uundaji, usambazaji na utumiaji wa vitabu.

Nyingine ni utekelezaji wa vitendo wa sera ya elimu ya kujifunza na ufundishaji shirikishi na kuchelewa  upatikanaji wa ithibati kwa vitabu vya ziada.

Akizungumza wakati akikabidhi msaada wa vitabu 30,0500 katika maktaba Kuu ya Taifa vyenye thamani ya zaidi ya Sh100 milioni, leo Jumatano Agosti 28,2019 amesema lengo la msaada huo ni kuongeza ufanisi wa maktaba hiyo kuwa na vitabu vya kutosha vitakavyoongeza maarifa na uelewa kwa jamii.

Kuhusu utekelezaji kwa vitendo wa sera ya elimu ya kujifunza na ufundishaji shirikishi amesema itafanikiwa endapo kutakuwa na vitabu vya kutosha na kubainisha kuwa kuna uhaba wa vitabu katika maktaba nchini.

“Tunaelewa kuwa maktaba zina mchango mkubwa ila changamoto ni kwamba zipo chache na zina uhaba wa vitabu kwa hiyo tunatarajia wenye shule iliwemo Serikali watahakikisha kuwa kila shule inakuwa na maktaba na zinakuwa na vitabu vya kiada na ziada vya kutosha,” amesema

Pia Soma

Akielezea kuhusu ucheleweshwaji na upatikanaji wa ithibati kwa vitabu vya ziada amesema, “kwa sasa inachukua muda wa miaka mitatu, kama wadau hatuwezi huondoa uhaba wa vitabu na kuhuisha wadau mbalimbali kwa mtindo huu.”

Akizungumza  baada ya kupokea msaada huo mkurugenzi mkuu wa maktaba ya Taifa,  Dk Alli Mcharazo amesema vitabu hivyo vitaziba pengo la uhaba wa vitabu hasa kwa lugha ya Kiswahili.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz