Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amedai kuwa kwa takribani asilimia 40, watumishi wa umma kwenye maeneo mbalimbali nchini wanashiriki kwa namna moja ama nyingine katika kufanya magendo.
Chalamila ametoa kauli hiyo mkoani Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza katika hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti ya doria ya kukabiliana na uhalifu baharini na kwenye maziwa makuu.
Hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya Bandari ya Dar es Salaam.
"Miezi michache tumeendelea kupambana na magendo katika ufukwe wa Bahari ya Hindi, hali ya magendo ipo na sio chini ya asilimia 40 na inasindikizwa na kuungwa mkono kabisa na baadhi ya watumishi wa umma". Amesema Chalamila
Kuhusu boti hiyo ya doria Chalamila amesema itakuwa na manufaa kwa mkoa wa Dar es Salaam kwani itasaidia kupunguza uhalifu mkubwa unaofanywa kwenye Bahari ya Hindi.