Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Burunge: Jumuiya hifadhi inayosimama kwa mtindo wa bajeti mabilioni

BURUNGEE Burunge: Jumuiya hifadhi inayosimama kwa mtindo wa bajeti mabilioni

Tue, 7 Jul 2020 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

*Iko na vijiji 10, kimoja kina Sh. mil. 500 *Vina shule, zahanati, nyumba za walimu...

NI nadra kwa kijiji kuwa na uwezo wa kutimiza huduma za kijamii kwa kutumia mapato yake, huku kikiwa na akiba Sh. milioni 500 benki zinazosubiri kupangiwa matumizi ya maendeleo.

Lakini, unapotembelea vijiji 10 vya Kata za Nkaiti, Mwada na Magara katika Tarafa ya Mbugwe wilayani Babati mkoani Manyara, utayaona makubwa ya huduma za kijamii kama majengo ya shule, nyumba za walimu, zahanati, vituo vya afya na ofisi za vijiji za kisasa, ni vigumu kupata mfano wake katika vijiji vingine.

Katika vijiji hivyo, pia kuna ushuhuda wa ujenzi wa majengo ya shule mpya na huduma nyinginezo za kijamii. Siri ya mafanikio hayo ni nini? Fedha zinazotokana na utalii, kwenye Jumuiya ya Hifadhi za Jamii (Burunge Wildlife Management Area -WMA).

Ni kwamba, kila kijiji kinanufaika na mgao wa mamilioni ya shilingi kwa ajili ya kutekeleza maendeleo yao kwa mujibu wa vipaumbele walivyojiwekea.

Nipashe ilifanya ziara ya kuchunguza kupata undani wa uhalisia huo kwa uwezeshaji wa Shirika la Internews chini ya Mtandao wa Waandishi wa Habari Duniani (Earth Journalist Network).

Sura pana ya manufaa hayo, imebainika kuwezeshwa kujiendeleza kielimu kwa ngazi mbalimbali kwa watoto kutoka familia zisizojiweza kiuchumi. Hapo kuna maana ya ngazi kama vyuo vya ufundi hadi kileleni vyuo vikuu.

Kimsingi, kitaifa kuna jumla ya jumuiya 38. Kati yake, 16 ndiyo zimesajiliwa, ambazo mbali na Burunge, nyinginezo ni Iyumbu, Ipole, Ikona, Makao, Enduiment, Wami Mbiki, Ukutu, Tunduru, Mbaragandu, Liwale, Ngarambe Tapika na Idodi Pagawa.

Burunge inashika nafasi ya pili kimapato ikikusanya Sh. bilioni 2.3, ikitanguliwa na Serengeti inayokusanya Sh. bilioni 2.7 kwa mwaka.

Katibu wa Jumuiya ya Burunge, Benson Maise, anafafanua utaratibu wa mgao wa mapato, kwamba nusu hubaki kwenye jumuiya kwa ajili ya shughuli za uendeshaji na kinachobaki hupelekwa kwenye vijiji 10 vilivyo katika ubia na hifadhi hiyo.

Tafsiri ya mafanikio yaliyoko vijijini, ni kwamba vinamiliki hoteli za kitalii zenye wateja mamia ya wageni hifadhini, ambazo manufaa yake yanaenda moja kwa moja kijijini.

Mfano hai wa mafanikio hayo, unaonekana katika Kijiji cha Sangaiwe chenye akiba ya Sh. milioni 500 benki kwa ajili ya matumizi kama vile ujenzi wa shule, zahanati na miradi ya barabara na maji.

Katibu huyo anafafanua vigezo vya mgao, inapotokea kijiji kinashindwa kutunza eneo la hifadhi, kinanyimwa fedha hizo hadi kitakaporekebisha kasoro zilizojitokeza.

Mafanikio yaliyopo hadi sasa, wakazi wa vijiji vyote 10 hawachangishwi fedha za miradi ya maendeleo kama ilivyowahi kujitokeza huko nyuma katika hatua za kujipanga walipochangisha Sh. 70,000 kwa kila kaya.

Maise anasema, kwa sasa akiba ipo na kinachofanyika ni fedha zinatumika kwa mujibu wa bajeti na mipango iliyopitishwa na mkutano mkuu wa kijiji.

DIWANI ANENA

Diwani wa Mwada, Gerald Chembe, ambako ndiyo makao makuu ya WMA, anasema vyombo vya usafiri vilivyopo, pia vinatumika kuwapeleka wanavijiji katika mahitaji kama hospitali, shughuli za kiuchumi na kijamii.

Chembe ambaye yumo katika waanzilishi wa WMA hiyo, anasema walianza na wazo la uchumi wa uhifadhi na wakalitekeleza kwa kutoa elimu kwa kushirikiana na Africa Wildlife Foundation, na wakapata mwitikio wa wananchi ambao waliridhia sehemu ya ardhi yao kuingizwa kwenye jumuiya.

"Tulianza kama hifadhi ya jamii, nami nilikuwa katibu wa kamati ya usimamizi wa mazingira. Tulipeleka baadhi ya wananchi kusoma, wakati huo tulikuwa tunatembea porini kwa miguu na baiskeli na bado baadhi walikuwa hawaoni umuhimu kwa kuwa waliendelea kukata miti na kulisha mifugo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live