Watu 20 wameripotiwa kupoteza maisha na wengine 15 kujeruhiwa kwenye ajali iliyohusisha magari matatu na Trekta katika eneo la Mwakata barabara ya Isaka Kahama mkoani Shinyanga.
Mashuhuda wa ajali hiyo wamesema ajali hiyo imetokea majira ya saa 4 usiku Jumatatu Agosti 8, 2022 ikihusisha gari ndogo aina ya Toyota IST yenye namba za usajili T880 DUE, gari ndogo ya abiria aina ya Toyota Hiace yenye namba za usajili T350 BDX, Lori pamoja Trekta.
Inaelezwa kuwa Toyota Hiace iligongana uso kwa uso na Lori/Scania yenye namba za usajili T658 DUW.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Hospitali ya Kahama watu 20 wamepoteza maisha na 15 kujeruhiwa katika ajali hiyo na majeruhi wanaendelea kupata matibabu.
"Watu 17 walipoteza maisha papo hapo eneo la tukio na watatu wamefariki baada ya kufikishwa hospitali, majeruhi wapo 15", taarifa inaeleza.
Mpaka sasa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga halijazungumzia kuhusu tukio hili, juhudi za kumtafuta Kamanda wa polisi zinaendelea.