Kibiti. Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) nchini Tanzania, Brigedia Jenerali Charles Mbuge amezindua kikosi kipya cha 830 cha jeshi wilayani Kibiti Mkoa wa Pwani huku akiwataka wakazi wa eneo hilo kuishi kwa upendo, ushirikiano na askari wa kikosi hicho kipya.
Brigedia Jenerali Mbuge amezindua kikosi hicho leo Jumamosi Oktoba 19, 2019 katika Kijiji cha Mkupuka kilichopo kata ya Mchuki wilayani Kibiti mkoani Pwani.
Mkuu huyo wa JKT, aliyeteuliwa Septemba 10, 2019 na Rais John Magufuli kushika nafasi hiyo, amewasisitiza wakazi wa Kibiti na wanaozunguka kikosi hicho kuishi kwa upendo na askari hao huku akikumbushia baadhi ya matukio ya mauaji yaliyojitokeza siku za nyuma katika wilaya hiyo.
"Tushirikiane kwa ushirikiano ikiwamo kutoa taarifa kwa uongozi na kijiji na kikosi hiki, mtakumbuka historia iliyokuwepo hapo awali. Baadhi ya watu wachache ambao hawakulitakia mema walikuwa wakifanya vurugu.”
"Vurugu hizo zilisababisha watu ambao ni nguvu kazi kupoteza maisha.Ni vyema wananchi mnaozunguka eneo la kikosi kudumisha amani sambamba na kutoa ushirikiano kwa viongozi," amesema Brigedia Jenerali Mbuge.
Brigedia Jenerali Mbuge amesema eneo la kikosi hicho kipya ni la kimkakati kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa vijana waliomaliza kidato cha sita sambamba na kuilimarisha ulinzi na usalama akiwa na matumaini watashirikiana na vyema na wakazi wa Kibiti.
Pia Soma
- Rais Magufuli ateua na kutengua, wamo DED, DC
- VIDEO: Mafuriko yafukua makaburi 20 Mwanza
- VIDEO: Tanzania kuzikutanisha nchi 48 za Asia na Afrika
Mbali na hilo, Mbuge amesema uwepo wa kikosi hicho kutakuwa na fursa na manufaa kwa wakazi wa Kibiti ikwemo kupata nafasi ya kupata mafunzo kwenye sekta za kilimo na ufugaji wa kuku na ng'ombe.
"Wananchi watapata fursa ya mafunzo kutoka kwa wataalamu wa jeshi. Pia, fursa za ajira endapo tutaanzisha viwanda katika eneo hili," amesema Mbuge.
Akizindua rasmi kikosi hicho, Brigedia Jenerali Mbuge amesema "Sipendi mtu mwenye maneno mengi napenda kazi tu. Mimi ni mkuu wa JKT wa 14 mmenipa pongezi lakini nazirudisha kwenu kwa kusisitiza uchapakazi na tuungane na Rais Magufuli.”
Kaimu kamanda wa kikosi hicho, Luteni Kanali Mohammed Karuma amesema kikosi hicho kitatoa fursa ya vijana kushiriki shughuli za ujenzi wa Taifa akisema ni tukio la kihistoria huku akiwashukuru uongozi wa wilaya Kibiti kuridhia eneo kutumika.