Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bilioni zatengwa kutengeneza madawati shule ya msingi

Be9af46626b7f37cac03e5ce2fd88db1.jpeg Bilioni zatengwa kutengeneza madawati shule ya msingi

Fri, 30 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SERIKALI imetenga Sh bilioni 7.15 kwa ajili ya kutengeneza madawati 710,000 katika shule za msingi katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati.

Hayo yalibainishwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, David Silinde wakati akijibu swali la Mbunge wa Tabora Mjini, Emmanuel Mwakasaka (CCM).

Katika swali lake la msingi, Mwakasaka alitaka kujua hatua gani serikali imechukua katika kukabiliana na tatizo la upungufu wa walimu na madawati hasa baada ya elimu ya msingi na sekondari kuwa bure.

Akijibu swali hilo, Silinde alisema serikali imeendelea kuajiri walimu wa shule za msingi na sekondari ambapo kuanzia mwaka 2016/17 hadi 2020/2021 jumla ya walimu 33,684 na mafundi sanifu maabara 497 wameajiriwa.

Silinde alisema Ofisi ya Rais-Tamisemi kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknoloja, itaajiri walimu 6,000 ifikapo Juni 30 mwaka huu.

Alisema ajira hizo ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa hivi karibuni.

"Ili kukabiliana na upungufu wa madawati katika mwaka wa fedha 2021/22, serikali imetenga shilingi bilioni 7.15 kwa ajili ya kutengeneza madawati 710,000 katika shule za msingi. Pia serikali inaendelea kushirikiana na Wadau wa Maendeleo pamoja na wananchi katika kutatua changamoto ya madawati kwenye shule za msingi na sekondari nchini,"alisema Silinde.

Chanzo: www.habarileo.co.tz