Mfanyabiashara wa madini ya Tanzanite nchini Tanzania, Saniniu Laizer amechangia Sh5 milioni za ujenzi wa ofisi ya chama cha walimu Tanzania (CWT) ili kuboresha utendaji kazi wa walimu.
Laizer maarufu bilionea Laizer ametoa fedha hizo leo Jumamosi Oktoba 30, 2021 kwenye semina ya walimu wawakilishi mahali pa kazi na kuendesha harambee iliyosaidia kupatikana Sh10 milioni.
Akizungumza baada ya kumkabidhi fedha hizo mwenyekiti wa CWT Wilaya ya Simanjiro, Abraham Kisimbi, mfanyabiashara huyo amesema jamii ya kifugaji inatambua mchango mkubwa wa walimu.
"ili walimu mfanye kazi zenu kwa ufanisi mkubwa ninawachangia Sh5 milioni muweze kuendelea na ujenzi wa ofisi ya chama chenu," amesema Laizer.
Mwenyekiti wa CWT wilayani Simanjiro, Abraham Kisimbi amemshukuru Laizer kwa kuwaunga mkono kwenye ujenzi wa ofisi yao kwani hivi sasa wamepangisha kwenye jengo la CCM wilayani humo.
Mwenyekiti wa CWT Mkoa wa Manyara, Wenceslaus Leo amewaagiza viongozi wa CWT wa wilaya hiyo waanze ujenzi wa ofisi zao mara moja.