SERIKALI kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imetenga Sh bilioni 7.3 kufungua barabara za Halmashauri ya Wilaya ya Iramba mkoani Singida ikiwa ni utekelezaji wa
kaulimbiu yake ‘Tunakufungulia barabara kufika kusikofikika’.
Akiwa katika ziara ya kikazi wilayani humo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu amesema azma ya serikali ni kufungua barabara za vijijini ili wananchi wafanye kazi zao bila kikwazo cha usafiri.
Akikagua barabara ya Shelui - Tintigulu inayojengwa kwa urefu wa kilometa saba, ameelekeza barabara hiyo ijengwe kwa ubora unaotakiwa ili idumu na kuwasaidia wananchi wa Shelui katika shughuli zao za kila siku.
Pia amemuelekeza Meneja wa Tarura Wilaya ya Shelui, Evance Kibona kuhakikisha kuwa wanafanya usanifu wa Daraja la Nshoka linalounganisha kata za Shelui - Tintigulu ili barabara hiyo inayojengwa ilete manufaa zaidi kwa wananchi wa maeneo hayo.
“Mto huu ni mkubwa na hakuna daraja sasa wakati wa mvua wananchi hawawezi kupita hapa hivyo ni vyema hapa pakajengwa daraja ili barabara hii iwe na tija stahiki,” alisema Ummy.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa barabara hiyo ya Shelui-Tintigulu, Meneja wa Tarura Wilaya ya Iramba, Evance Kibona alisema
ujenzi wa barabara hiyo umeanza Desemba 11 na utakamilika Juni, 2022.
Kwa mwaka wa fedha 2020/21, bajeti ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Iramba ilikuwa milioni 860 na katika mwaka wa fedha 2021/22 bajeti hiyo imeongezwa mpaka kufikia Sh bilioni 7.3.