Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Bil. 22 kuweka lami barabara 20 za mji wa Songea

Bil. 22 Kuweka Lami Barabara 20 Za Mji Wa Songea Bil. 22 kuweka lami barabara 20 za mji wa Songea

Fri, 7 Jun 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma ni miongoni mwa Halmashauri 12 nchini ambazo zimepata mradi wa uboreshaji wa miundombinu ya barabara za lami nzito ili kuboresha miundombinu ya miji,manispaa ya majiji.

Akitoa taarifa ya mradi huo kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Ahmed Abbas,Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea Wakili Bashir Muhoja amesema katika Manispaa hiyo barabara za lami zenye urefu wa kilometa 10.1 zitajengwa ambapo jumla ya barabara 20 za katikati ya mji zitatengenezwa kupitia mradi huo.

Amesema Zaidi ya shilingi bilioni 22 zinatekeleza mradi huo ambao umefadhiliwa na Jumuiya ya Maendeleo ya Kimataifa (IDA) kupitia Benki ya Dunia ili kuboresha miundombonu na ushindani wa miji,manispaa na majiji nchini Tanzania.

Amebainisha kuwa mradi umeanza kutekelezwa ambapo hivi sasa mkandarasi amefikia asilimia 8.3 ya utekelezaji ujenzi wa barabara na ujenzi wa ofisi ya TARURA umefikia asilimia 18 ambapo mradi unatarajia kukamilika Februari 2025.

“Tunaishukuru sana serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia mradi huo muhimu wa kuboresha miundombinu ya barabara za lami mjini Songea’’,alisema.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo ,Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Ahmed Abbas Ahmed ameishukuru serikali na wadau wengine wa maendeleo kwa kutenga fedha za kutekeleza mradi huo ambao unakwenda kuboresha barabara za lami za mji wa Songea.

Hata hivyo kutokana na mradi huo kuwa nyuma ya mkataba amemshauri Mkandarasi kuongeza nguvu kazi na vifaa ambapo ameyataja madhumuni ya miradi inayotekelezwa na serikali ni kuleta chachu ya maendeleo kwa wananchi hivyo kuchelewa kutekelezwa kwa miradi kuna punguza kasi chachu.

“Mkoa wa Ruvuma ni wazalishaji wakubwa wa chakula nchini ambacho kinapelekwa kwenye mikoa mingine na nje ya nchi,tungetarajia kuiona kasi ya ukuaji wa Mkoa inalingana na hali ya mambo inayoyafanya,watu wanatamani kuona utekelezaji wa shughuli za kijamii zinafanyika kwa kasi kubwa’’,alisisitiza Kanali Abbas.

Hata hivyo amesema hajafurahishwa na utekelezaji wa mradi huo kwa kiwango kilichofikiwa kwenye mradi huo hivyo ameagiza mradi huo utekelezwa kwa kasi ili wananchi waanze kunufaika na mradi huo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live