Dar es Salaam. Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) leo Jumamosi Mei 18, 2019 imeteketeza bidhaa bandia zenye thamani ya zaidi ya Sh650 milioni zilizokamatwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Uteketezaji wa bidhaa hizo umefanyika katika kiwanda cha kuthibiti taka cha Tindwa Medical and health service kilichopo wilayani Kisarawe Mkoa wa Pwani.
Bidhaa zilizoteketezwa ni vipuri vya magari na pikipiki, mashine za kusukuma maji, vilainishi vya mitambo, vipodozi, mikoba, wino wa kuchapisha nyaraka za ofisi, vifaa vya kujikinga vumbi na kung’arisha viatu.
"Sheria inaelekeza tukishakamata tunateketeza au kugawa kwa taasisi lakini sio kwa matumizi ya biashara na bidhaa hizi leo tumeona zinafaa kuteketezwa na sio kutumiwa na watu tena," amesema Dk John Mduma, mkurugenzi wa FCC.
Amebainisha wanaoingiza bidhaa bandia wanakwepa udhibiti wa vyombo vingine kama TBS na Mamlaka ya Udhibiti wa Chakula na Dawa (TFDA) wakati wakijua bidhaa hizo si salama kwa matumizi ya binadamu akitolea mfano kofia ngumu na vipuri vya magari.
"Tunapodhibiti lengo letu sio kuongeza umasikini kwa watu bali tunalinda walaji ili wasiathirike na matumizi ya bidhaa hizo lakini pia tunalinda viwanda vinavyozalisha bidhaa halisi," amesema.
Pia Soma
- Karanga mbichi, mhogo, nazi haviongezi nguvu za kiume
- Aliyesifiwa bungeni apandishwa cheo CRDB
- Walichokisema wananchi majibu ya Membe kwa Rostam
"Sisi kampuni yetu inatengeneza mafuta yaitwayo Bio oil hatuna bidhaa nyingine lakini hapa kuna sabuni na lotion inayotumia jina letu na chapa yetu, inaonyesha imetengezwa Afrika Kusini ambako mafuta yetu yanatengenezwa lakini bidhaa hizi zinatoka China," amesema.