Dar es Salaam. Wakati Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi akiagiza polisi kumkamata popote alipo Katibu wa Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) wilaya Temeke, Hilda Newton, uongozi wa baraza hilo umesikitishwa na hatua ya mkuu huyo wa mkoa.
Katika taarifa yao kwa vyombo vya habari waliyoitoa leo, Katibu Mwenezi wa Bavicha, Edward Simbeye amesema wamesikitishwa na kitendo cha Hapi kumwita Hilda ;mtu mfupi’ kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter.
Simbeye amedai Hapi alifika mbali katika taarifa aliyotoa jana akimtaka Hilda kuripoti kwa kamanda wa polisi wa mkoa huo ambapo alimdhihaki kwa maumbile yake kwa kumuita binti mfupi wa Bavicha.
Soma zaidi: Hilda wa Chadema amgomea RC Hapi
Simbeye katika taarifa yake ameueleza umma kauli aliyoitoa Hapi katika mtandao huo wa kijamii ni batili na hana mamlaka hayo kwa mujibu wa sheria na Bavicha inamtaka afuate utaratibu uliowekwa kisheria vinginevyo arejee kwenye miongozo ya mamlaka yake.
“Bavicha tunafuatilia kwa karibu suala hili ili kuhakikisha haki zote za msingi zinapatikana kwa Hilda dhidi ya Hapi. Hatutakuwa tayari kuona aina yoyote ya uonevu inafanyika dhidi yake,” amesema Simbeye.
Soma zaidi: RC Hapi aagiza polisi kumkamata Hilda wa Chadema popote alipo
Soma zaidi: Kauli ya RC Hapi kuhusu Hilda wa Chadema yamuibua Zitto, Mchungaji Msigwa