Dodoma. Serikali ya Tanzania imeombwa kuipokea taarifa iliyovuja ya Shirika la Fedha Duniani (IMF) kwa kuwa ina mambo mazuri.
Kauli hiyo imetolewa bungeni leo Jumanne Mei 14, 2019 na Mbunge wa Nzega Mjini (CCM), Hussein Bashe wakati akichangia hotuba ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka 2019/20.
Katika mchango wake Bashe amesema taarifa hiyo ni dira ya kuisaidia Serikali katika kujipanga vizuri zaidi kwani kuna mambo mazuri ndani yake.
Akizungumzia suala la viwanda amesema wafanyabiashara Tanzania wanapata shida kubwa katika uanzishaji wa viwanda kutokana na utitiri mkubwa wa kodi.
Bashe ametolea mfano kwa mtu anayeanzisha kiwanda cha madawa, anapaswa kuwa na leseni 26 sawa na anayeanzisha kiwanda cha maziwa.
Ameshauri taasisi nyingi kuweka kambi pamoja na kuwaondolea usumbufu wafanyabiashara wanaotaka kufungua biashara.
Habari zinazohusiana na hii
- Dk Mpango ataka ripoti ya IMF iliyovuja kupuuzwa
- Silinde, Zitto walivyochuana na mawaziri wa Fedha ukuaji wa uchumi