Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Barakoa, ‘Levo siti’ sasa lazima Dar

29a7cd60ab38ebc8ef5f4900d725f9c1 Barakoa, ‘Levo siti’ sasa lazima Dar

Tue, 3 Aug 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

MKUU wa Mkoa (RC) wa Dar es Salaam, Amosi Makalla, amesema kuanzia sasa suala la abiria katika vyombo vya usafi ri kukaa kulingana na idadi ya viti (levositi) na matumizi ya barokoa katika ofisi za umma si hiari, bali ni lazima.

Ameagiza wamiliki wa vyombo vya usafiri kutoruhusu watu wasiovaa barakoa kupanda katika vyombo vyao vya usafiri kuanzia sasa.

Alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya Kikao cha Tathmini cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa kujadili mwenendo wa maambukizi ya virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa wa homa kali ya mapafu maarufu, Covid-19 katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Alisema vyombo vyote vya usafiri vinapaswa kufuata taratibu za miongozo ya afya ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona huku wakizingatia kuwa, kuanzisa sasa suala la abiria kukaa kulingana na idadi ya viti ni lazima.

“Kuanzia sasa naagiza wamiliki wote wa vyombo vya usafiri wasiruhusu mtu yeyote asiyevaa barakoa kupanda katika chombo cha usafiri au kuingia katika ofisi yoyote ya umma ;au usafiri wa mwendokasi na vivuko,” alisema Makalla.

Aidha, alisema katika utekelezaji wa agizo hilo, kila basi wataingia wanafunzi watano wakiwa wamevaa barakoa ili kuepusha msongamano.

Alisema mbali ya kuvaa barakoa ni muhimu kila mtu kuepuka mikusanyiko isiyokuwa ya lazima huku akitolea mfano wa sherehe za harusi na mikutano ya kisiasa kwa kuwa hali ya maambukizi ya ugonjwa huo ni mbaya na watu wanaendelea kuambukizana.

Alisema kwa sasa mikutano ya kisiasa ni marufuku katika Mkoa wa Dar es Salaam na wilaya zake zote za Ilala, Kigamboni Kinondoni, Temeke na Ubungo.

Aliwataka wakuu wa wilaya za Mkoa wa Dar es Salaam kusimamia utekelezaji wa agizo hilo kwa kushirikiana na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Kwa mujibu wa RC Makalla, kuanzia sasa vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama vitafanya ukaguzi wakati wowote kuona utekelezaji wa agizo hilo.

Wakati huo huo: RC Makalla amesema maombi ya wahitaji wa chanjo katika Mkoa wa Dar es Salaam ni mengi ulinganisha na dozi 160,000 za chanjo zilizopokelewa katika mkoa huo.

Chanzo: www.habarileo.co.tz