Dodoma. Ujenzi wa barabara za mzunguko katika Jiji la Dodoma zenye urefu wa kilomita 112.3 utafanyika kwa miezi 36 huku Sh17 bilioni zikitengwa kuwalipa wananchi fidia.
Kiasi cha Sh494 bilioni za ujenzi wa barabara hizo kitatolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika na Serikali ya Tanzania.
Akizindua ujenzi huo leo Jumanne Oktoba 29, 2019 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe amesema Tanzania itatoa Sh82 bilioni.
“Fidia itafanyika kwa mujibu wa sheria za nchi. Tunawaomba wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha katika mradi huu," amesema Kamwelwe.
Patrobas Katambi, mkuu wa Wilaya ya Dodoma akizungumza kwa niaba ya mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge amesema Mkoa utasimamia ulipaji fidia kuhakikisha kila kinachohitajika katika ujenzi huo kinapatikana.
Mtendaji mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Patrick Mfugale amesema uombaji zabuni kwa ajili ya makandarasi wa ujenzi wa barabara hiyo utafunguliwa Desemba 12, 2019, kwamba ujenzi huo utafanyika kwa miezi 36.
Pia Soma
- Alipa Sh13 milioni kwa kukisababishia hasara Chuo Kikuu Huria
- Uturuki yaapa kushambulia wapiganaji wa Kikurdi
- Takwimu wanaopata ulemavu baada ya kuugua kiharusi zatajwa