Handeni. Barabara kuu ya kutoka Dar es Salaam kwenda mikoa ya Kaskazini ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara na nchi jirani ya Kenya imefunguliwa leo Jumatatu Oktoba 14, 2019 kuanzia saa 12 jioni.
Ilifungwa jana kutokana na magari kushindwa kupita katika daraja la mto Mnyuzi kijiji cha Mandera wilaya ni Handeni, ilifungwa na polisi kwa sababu ya usalama.
Akizungumza na Mwananchi leo Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Tanga, Solomon Mwangamilo amesema wameanza kuruhusu magari madogo kupita.
Amesema kwa sasa maji yamepungua lakini hawaruhusu magari makubwa ambayo yanatakiwa kupita Handeni mjini hadi Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) watakapojiridhisha daraja hilo lipo salama.
"Tumeanza kuruhusu magari madogo kupita tangu saa 12 asubuhi ila tunaendelea kufuatilia ili lisitokee tatizo lolote na kusababisha madhara, tutatoa taarifa zaidi baadaye". amesema Mwangamilo.