Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Barabara Mkoani Kigoma kumulikwa

Kigz Road Sehemu ya barabara inayojengwa Mkoani Kigoma

Mon, 28 Feb 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakandarasi wanaotekeleza mradi wa ujenzi wa barabara ya Manyovu – Kasulu – Kibondo – Kabingo kwa kiwango cha lami yenye jumla ya urefu wa KM 260.6 wametakiwa kukamilisha barabara hiyo kwa kuzingatia ubora kama ilivyosanifiwa ili iweze kudumu kwa kipindi kirefu.

Wakandarasi hao ni CHICO anayetekeleza sehemu ya Njia panda ya Nduta – Kabingo KM 62.5, Sinohydro Corporation anayetekeleza sehemu ya Njiapanda ya Nduta – Kibondo Mjini KM 25.9 na Stecol Corporation anayetekeleza sehemu ya Mvugwe – Njiapanda ya Nduta KM 59.35.

Hayo yamesemwa mkoani Kigoma na Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi anayesimamia Sekta ya Ujenzi, Eng. Godfrey Kasekenya, wakati alipowasili mkoani humo na kukagua maendeleo ya mradi huo.

“Tunategemea barabara hii ikikamilika kujengwa matengenezo yake yaanze baada ya miaka 20 hivyo basi TANROADS kwa niaba ya Serikali hakikisheni mnawasimamia wakandarasi hawa ili tupate barabara yenye viwango vya juu”, amesisitiza Eng. Kasekenya.

Aidha, ameagiza wakandarasi hao kuongeza muda wa kazi na vifaa ili kukamilisha mradi huo mapema zaidi ili kufungua mkoa wa Kigoma kwa barabara za lami.

“Serikalii itaendelea kulipa fedha za mradi kwa wakati sasa ni jukumu lenu kuongeza muda wa kazi ili kutoongeza gharama za mradi”, amesema Eng. Kasekenya.

Eng. Kasekenya ameeleza umuhimu wa barabara hiyo inayounganisha mtandao wa barabara za Afrika Mashariki kutokea Nyakanazi kwenda Kigoma kupitia makao makuu ya wilaya ya Kibondo ikIunganisha Kasulu hadi Manyovu kwa kiwango cha lami na kutoka Kasulu hadi Burundi kwa barabara ya lami.

Ameongeza kuwa tayari wakandarasi wapo eneo la kazi kutokea Kigoma ukielekea Tabora kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Uvinza – Malagarasi KM 51.1 na Kazilambwa – Chagu KM 36 kwa kiwango cha lami

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Kigoma Eng. Suleiman Bishanga, amemueleza Naibu Waziri huyo kuwa mpaka maendeleo ya ujenzi wa barabara sehemu ya Njia panda ya Nduta – Kabingo KM 62.5 imefikia asilimia 20 na unagharimu shilingi Bilioni 95.5 sehemu ya Njiapanda ya Nduta – Kibondo Mjini KM 25.9 imefikia asilimia 42.1 na unagharimu shilingi Bilioni 31.0 na sehemu ya Mvugwe – Njiapanda ya Nduta KM 59.35 imefikia asilimia 29.1.

Utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Manyovu – Kasulu – Kibondo – Kabingo kwa kiwango cha lami KM 260.6 umegawanywa kwa sehemu nne ambazo ni Njia panda ya Kasulu – Manyovu na viunganishi vya barabara za Kasulu mjini KM 68.25, Kanyani – Kidyama – Mvugwe KM 70.5, Mvugwe – Njia panda ya Nduta KM 59.35 na Njia panda ya Nduta – Kabingo KM 62.5.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live