Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wa Wilaya ya Babati, Mhandisi Bakari Mwanyiro, alisema mradi huo umekuwa mkombozi kwa wakazi hao, kwa kuwa idadai kubwa ya wanawake na watoto walisota nyakati za usiku kuhemea maji ya kunywa.
“Hili tatizo limemalizika, baada ya mpango wa serikali wa kumtua mama ndoo kichwani kuzaa matunda. Adha ya kutafuta maji usiku wa manane sasa haipo, mmeuona mradi wa Nangara na mingine inavyofanya vizuri,”alisema
Kwa mujibu wa Mhandisi Mwanyiro, hali ya upatikanaji wa maji kwa wilaya hiyo ni asilimia 73 na vijiji ni asilimia 75. Kwa sasa vijiji 102 pekee ndivyo, vyenye uhakika wa huduma ya maji.
Aidha, alisema RUWASA inatarajia ifikapo mwaka 2025, upatikanaji wa maji uwe umefika asilimia 85 kwa vijijini kama ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) inavyoelekeza.