Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Askari adaiwa kuvunja mguu raia

Mjdl Polisi.jpeg Askari adaiwa kuvunja mguu raia

Sun, 8 Jan 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Licha ya hila za askari polisi kutaka kumfichia siri mkuu wao, jitihada binafsi za Hidaya Somba zilisaidia kutambua alikofichwa mwanaye, Mohamed Khatibu (29) aliyekamatwa akiwa nyumbani kwao kwa tuhuma ambazo hazikubainishwa na alipofuatiliwa ikaelezwa hayupo mikononi mwa polisi.

Taarifa zilizothibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Gideon Msuya zinasema Khatibu alikamatwa Januari 3 na Mkuu wa Kituo kidogo cha Polisi Kiseke kilichopo wilayani Ilemela, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Paulo ambaye anadaiwa kumvunja miguu na kiuno akimtuhumu kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mzazi mwenzake.

Katika ukamataji, askari huyo ambaye ametoroka na sasa anatafutwa, anadaiwa kushirikiana na rafiki yake, wakitumia gari binafsi waliloenda nalo nyumbani kwa Khatibu katika Mtaa wa Mlimani A na kumkamata bila kumweleza kosa lake wakisema wanampeleka Kituo cha Polisi Kirumba ambako ndugu walipofuatilia hawakumkuta, kwani alipelekwa Kiseke.

Kituoni hapo alipigwa akihojiwa kwa nini ana uhusiano na mke wa mkuu huyo wa kituo mpaka akavunjwa vikombe vya magoti na majeraha kwenye uti wa mgongo kama ilivyothibitishwa na vipimo alivyofanyiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando.

Kamanda Msuya alisema japo mtuhumiwa namba moja katika tukio hilo ametoroka, uchunguzi unaendelea na hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaothibitika kushiriki uhalifu huo.

VIDEO: Askari adaiwa kuvunja raia miguu

“Primary suspect (Paulo) kwenye tukio la mtu kushambuliwa ametoroka na tunaendelea kumtafuta, uchunguzi ukikamilika wahusika watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria sawa na watuhumiwa wengine,” alisema Msuya.

Mama alivyompata

Paulo akiwa na rafiki yake, walimkamata Khatibu saa 5:00 asubuhi. Kutokana na kutoeleza sababu walibishana kidogo, lakini dada yake aitwaye Saida Khatibu aliyekuwepo nyumbani alimsihi akubali akiahidi kufuatilia Kituo cha Polisi Kirumba.

“Familia yangu ilipata imani kuwa watu wale ni askari polisi kwa sababu walikuwa na pingu na walidai wananipeleka Kirumba lakini tulikipita kituo hicho na wakanipeleka Kituo cha Polisi Kiseke. Nilipofikishwa pale kituoni nilifungwa kitambaa cheusi na pingu mikononi, na kuanza kushushiwa kipigo, ndipo nikapelekwa mahabusu bila taarifa zangu kuandikishwa, damu zilikuwa zikinivuja magotini, kwenye kifundo cha miguu na nyayoni,” alisema.

Alipopata taarifa za mwanaye kukamatwa, Hidaya alienda Kituo cha Polisi Kirumba lakini hakumkuta, hivyo akaanza kuzunguka kwenye vituo vingine vya polisi Wilaya ya Ilemela na Nyamagana bila mafanikio.

“Baadaye tulipata fununu kuwa aliyemkamata ni mkuu wa Kituo cha Polisi Kiseke, ikabidi twende huko, lakini askari waliokuwepo walitueleza Mohamed Khatibu hakuwepo kituoni hapo, lakini kutokana na uhakika niliokuwa nao, nilijifanya naenda chooni, nikazunguka nyuma ya mahabusu na kuita jina kwa sauti, naye akaitikia akiwa mahabusu,” alisema mama huyo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live