Sengerema. Raulensia Isamalaja (28) mkazi wa kata ya Nyatukala wilayani Sengerema mkoani Mwanza amenusurika kifo baada ya nyumba waliyokuwa wakiishi kusombwa na maji jana wilayani Sengerema kutokana na mvua iliyonyesha zaidi ya saa matano.
Isamalaja amesema wakati mvua ilipoanza kunyesha jana na maji kuanza kujaa alimwambia mpangaji mwenzake Veronica Magwendela (33) waondoke ndani ya nyumba hiyo kabla madhara hayajatokea lakini mama huyo alikataa hadi mauti yalipomkuta yeye na wanae wanne.
Amesema aliowashuhudia wakipoteza maisha kwa kuangukiwa na nyumba waliyokuwa wakiishi ni Veronica na watoto wake wanne ambao ni Kanguji Shinje, Fransinco Shinje, Edward Shinje na Edward Shinje.
“Kabla mauti hayajamkuta nilimwambia tuondoke ndani ya nyumba hakukubali na aliniambia mimi niendee tu, muda kidogo maji yalijaa na mvua kuzidi kunyesha, nyumba ikaanguka na wote wakafa, nililia kwa kuomba msaada kuwaokoa lakini nilishindwa,” amesema Isamalaja.
Zakaria Muhung'wa ni mjomba wa mama Veronica Magwendela aliyepotaza maisha na wanae wanane alifika eneo la tukio na kujionea hali halisi huku akisubiri taratibu za Serikali ili wapatiwe miili hiyo wakazike nyumbani kwao kijiji cha Kasalazi mkoani Geita.
Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Emmanuel Kipole amesema hadi sasa hakuna miili mingine iliyogundulika bado ni watu kumi na watu watano waliojeruhiwa na wamelazwa hospitali ya Wilaya ya Sengerema wakipatiwa matibabu na miili hiyo bado imehifadhiwa kisubili taratibu za maziko.
Katika hatua nyingine wakazi wa Sengerema waliojenga mabondeni wameanza kuondoka kwenye maeneo ya mabondeni kutii agizo la mkuu Wilaya ya Sengerema kuondoka kwenye maeneo hayo ilu kunusuru maisha yao.