Dodoma. Baraza la Vyama na Maendeleo ya Jamii (Tacosode) lipo katika hatua za mwisho kukamilisha kitini cha kufundishia Jamii, Azaki na watendaji wa Serikali.
Kitini hicho kitatoa ufafanuzi kuhusu mfumo wa ufuatiliaji wa Uwajibikaji Jamii (MUUJ) utakaowezesha asasi za kiraia nchini Tanzania kuwa na mfumo mmoja wa ufuatiliaji.
Mratibu wa mradi wa Tacosode, Koga Mihama amesema leo Machi 26, 2019 kuwa uandaaji wa kitini hicho umeshirikisha asasi za kiraia zilizofanya miradi ya ufuatiliaji na uwajibikaji jamii, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na watendaji wa halmashauri.
"Rasimu ya kwanza iliyoandaliwa na asasi zinazojishughulisha na miradi ya ufuatiliaji na uwajibikaji nchini na baadaye inapelekwa Tamisemi," amesema.
Amebainisha kuwa kabla ya kuwepo kwa kitini hicho asasi za kiraia zilikuwa kila moja na mfumo wake wa kuendesha miradi lakini sasa kutakuwa na usawa katika ufuatiliaji na uwajibikaji.