Arusha. Jiji la Arusha nchini Tanzania limeanza operesheni ya kuyafanyia usafi magari ya abiria kwa kuyapulizia dawa ya kuzuia virusi ugonjwa wa corona.
Shughuli ya kuyapulizia dawa imeanza leo Ijumaa Machi 27,2020 na kuongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Fabian Daqarro.
Mabasi yote yanayotoka Jiji la Arusha kwenda mikoa mingine na yanayotoa huduma ndani ya jiji yamefanyiwa usafi huo.
Sambamba na mpango huo wa jiji, chama cha wasafirishaji abiria Arusha na Kilimanjaro (Akiboa) na wadau wa usafirishaji wametoa vifaa vya kujikinga na corona vikiwapo vitakasa mikono pamoja na dawa za kupulizia vyombo vya usafiri vyenye gharama zaidi ya Sh10 milioni kusaidia kinga dhidi ya corona ambayo hadi leo Tanzania imeripoti wagonjwa 13.
Daqaro amesema wataendekea na operesheni hiyo ya usafi kwa kushirikiana na wadau ambao tayari wameanza kutoa michago.
Amewataka wananchi wasiwe na taharuki na kuzusha maneno juu ya ugonjwa huo na waachie wataalamu wa afya kuweza kutoa taarifa pamoja na elimu.
Pia Soma
- Habari Maalum-Egazeti
- Balozi Kairuki: Wanafunzi wa Tanzania wanaosoma China wasirejee nchini humo
- Mabasi yanayoingia, kutoka Dodoma kupuliziwa dawa
"Kuna watu wanadhana potofu kuwa corona haiwezi kuwapata watu weusi hayo ni mawazo potofu kikubwa ni kufuata maagizo ya wataalamu wetu wa afya," amesema
Naye mganga mkuu wa Jiji la Arusha, Dk Kheri Kagya amesema ni vyema wasafirishaji wote wahakikishe abiria wanatumia vitakasa mikono kabla ya kupanda chombo cha usafiri ili wafike salama bila maambukizi ya ugonjwa huo.
Amesema maeneo ya stendi yana uwezekano mkubwa wa kuambukizana hivyo jukumu kuu ni kunawa mikono na kuepukana misongomano isiyo ya lazima kwani itasaidia kuepukana na janga Hilo.
Mwenyekiti wa Akiboa, Locken Adolf amesema shughuli hiyo ya upuliziaji dawa vyombo vya usafirishaji ni endelevu na litahusisha usafiri wa bodaboda, magari makubwa na madogo.
"Akiboa tutaendelea kushirikiana na serikali katika vita dhidi ya ugonjwa huu," amesema Adolf