Serengeti. Mwanafunzi wa kidato cha pili katika Sekondari ya Mugumu amelazwa kwenye Hospitali Teule ya Nyerere akiuguza majeraha baada ya kunusurika kunaswa na umeme wakati akikata mti.
Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumatatu Aprili 29,2019, David Geofrey (17), mkazi wa kijiji cha Kisangura, akiwa hospitalini hapo amesema apata ajali hiyo Aprili 28, saa 8 mchana.
"Nilikuwa nakata mlingoti wa katani, ulipokatika ukaegemea waya wa umeme nikiwa nimeushika huku ninapanga ambalo sehemu moja haina mpini nikajikuta nimepigwa shoti na kuanguka chini," amesema.
Akizungumza taratibu, amesema chini kulikuwa na unyevunyevu na alishangaa viatu alivyokuwa amevaa vilitoka kwenye miguu na ana majeraha katika miguu yote.
"Kilichosaidia mti huo ulianguka chini ndipo nikapata nafuu, kama ungeendelea kugusa waya ningekufa maana nilikuwa nimeishiwa nguvu kabisa," amesema.
Muuguzi wa zamu, Jonh Nyang'ombe amesema majeraha makubwa aliyoyapata yapo kwenye mikono na miguu na wanaendelea kumpa dawa.