Dar es Salaam. Mahakama ya Wilaya ya Ilala imemuachia huru mshtakiwa Neema Athuman (60) aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya jinai namba 180/2018 akidaiwa kumpiga Amina Abdallah (80).
Katika kesi hiyo, Neema anadaiwa kumpiga ngumi mbili Amina katika ugomvi uliotokea baina yao.
Hakimu Mkazi, Catherine Kihoja alitoa hukumu hiyo leo Alhamisi Mei 23, 2019 baada kupitia ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka na utetezi na kumuona mshtakiwa huyo hana hatia.
Hiyo ilitokana na upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha shtaka hilo pasipo kuacha shaka yoyote.
Upande wa mashtaka katika kesi hiyo uliwakilishwa na wakili wa Serikali, Grace Lwila.
Katika kesi hiyo Neema anadaiwa Februari 23,2017 Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam alimpiga Amina kitendo ambacho ni kinyume cha sheria.