Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amewapongeza viboko wa Mkoa wa Katavi waliohamia kwenye bwawa lililochimbwa katika mji wa Mpanda baada ya mto waliokuwa wakikaa kukauka.
Rais Magufuli ametoa pongezi hizo leo Ijumaa Oktoba 11, 2019 na kuzitaka mamlaka mkoani humo kushirikiana na Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) kuchimba mabwawa ndani ya Hifadhi ya Katavi kwa ajili ya wanyama hao.
Rais ametoa kauli hiyo kufuatia maagizo aliyoyatoa jana kwa Tanapa kujaza maji katika mto waliopo viboko hao na leo amesema tayari maji yameshaanza kujazwa.
“Hapa mjini kuna bwawa lilichimbwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu, kwa hiyo wale viboko wamekosa maji wamehamia kwenye bwawa lenu la mjini. Wale viboko hawajakosea, kwanza nawapongeza sana, wana akili sana. Wana akili kweli,” amesema Rais Magufuli.
“Nasikia mlikuwa mnataka kutoa maagizo wale viboko wauliwe hapana. Wale viboko wamekuja mjini, kwanza mmewazibia maji kule lakini pili Tanapa hawajawachimbia mabwawa.”
Ameongeza, “Kwa sababu Tanapa wangekuwa na akili kama viboko walivyo na akili wangewachimbia mabwawa mle ndani wale viboko wasingeondoka kwa sababu kule kuna majani wangeyapata kwa ajili ya ku-protect maisha yao. Lakini mlivyo mkachiba bwawa mjini kwa hiyo wakawafuata huko.”