Baraka Mayala (24) mkazi wa manispaa ya Shinyanga amenusurika kifo baada ya kukatwa mapanga wakati akitoka harusini na kuporwa simu na Sh10,000.
Tukio hilo limetokea Oktoba 7, 2022 ambapo katika maelezo yake Mayala amesema watu hao ambao hawafahamu waliokuwa zaidi ya 10.
"Nilipokuwa natoka harusini watu hawa walinivamia na kuanza kunikagua kwenye mifuko wakati nikijitetea ndipo wakaanza kunishambulia kwa mapanga na wamenikata kichwani mara mbili na nilipotaka kukimbia walinikata katika miguu yangu, na nilipotaka kutambaa kwa mikono walinikata mikononi kisha wakachukua Sh10,000 na simu ya mkononi wakakimbia."
Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya rufaa mkoani Shinyanga, Dk Kambi Buteta amethibitisha kumpokea kijana huyo hospitali na wanaendelea kumpatia matibabu.
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga, Jackson Mwakagonda amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kubainisha kuwa upelelezi unaendelea kubaini wahusika.