Dar es Salaam. Mkulima wa Mpunga kutoka Dakawa mkoani Morogoro, Veronica Anael amesema aliweza kubadilisha mfumo wa kuzamani wa kilimo baada ya kupata mafunzo kwa msaada wa Shirika la Misaada la Watu wa Marekani (Usaid).
Akizungumza na MCL Digital katika Ukumbi wa Kisenga kwenye Jukwaa la Fikra linalojadili kuhusu ‘Kilimo ni Maisha’ usiku huu wa Alhamisi Mei 23, 2019, Anael amesema awali alikuwa analima mpunga kwa ajili ya chakula tu na wakati mwingine haukutosheleza mahitaji yake.
Amesema kwa sasa huvuna gunia za mpunga kuanzia 30 hadi 50 pamoja na mazao ya mbogamboga ambayo yamemsaidia kujikimu kiuchumi.
“Nimeweza kuendesha maisha yangu, nawasomesha wajukuu zangu hata kukarabati nyumba yangu, kilimo kimeniinua kiuchumi,” amesema.
Amesema wakati anaposubiri mazao ya nafaka yakomae shambani, huwa analima mbogamboga na kuziuza.
“Nilisaidiwa na USAID nikaachana na kilimo cha kizamani cha pembejeo duni, walituelimisha wakatupatia mitaji, nafurahi kuachana na kilimo kisicho na tija,” amesema Anael.
Pia Soma
- Ansaf yataja suluhisho la changamoto tano za Kilimo
- Changamoto kuu za wakulima zawekwa wazi
- Mtafiti wa kilimo ayataja maeneo matatu yanayoweza kufanikikisha sekta ya kilimo Tanzania
- Licha ya changamoto kilimo, bado kinasonga mbele – Profesa Nyange