Kibaha. Watu watatu wamefariki dunia mkoani Pwani, wawili kati yao katika ajali ya basi iliyojeruhi wengine wanane.
Basi hilo mali ya kampuni ya Modern Coach lililokuwa likitokea Nairobi kwenda Dar es Salaam, liliacha njia na kupinduka.
Ajali hiyo imetokea jana Ijumaa Agosti 3, 2018 saa 5.45 usiku katika Kijiji cha Kimange kwenye barabara ya Segera - Chalinze.
Akizungumza leo Jumamosi Agosti 4, 2018, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Blasius Chatanda amewataja waliofariki dunia kuwa ni Aliakimu Mkiganda (41) mfanyabiashara ambaye ni raia wa Rwanda na Emmanuel Indimuli (3) raia wa Kenya. Miili yao imehifadhiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Amesema majeruhi katika ajali hiyo ni Penina Wango (33), Aliasgher Morbiwalia (18), Adrian Flovick (19), Mohamed Idris (18) Mita Naidhukum (54), Adrin Maula (16), Erick Muthon (30) na Hemik Muthon (49) wote raia wa Kenya.
Amesema majeruhi wote walipelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa matibabu.
Amesema dereva wa basi hilo amekimbia na juhudi za kumsaka zinaendelea ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake.
Katika tukio jingine, amesema mwendesha pikipiki Idd Bakar (20), amefariki dunia baada ya kugongana na basi mali ya kampuni ya ABC lililokuwa linatokea Dar esalaam kwenda Mailimoja, Kibaha.