Dar es Salaam. Wanafunzi watano wa shule ya msingi Ndelenyuma Halmashauri ya Madaba Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma wamefariki baada ya kugongwa na gari jana Jumatano Februari 12, 2020.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Februari 13, 2020 Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Simon Maigwa amesema ajali hiyo ilihusisha gari ndogo iliyokua na watu wawili waliokuwa wanakwenda kufanya ukarabati wa mnara.
“Wanafunzi sita waligongwa, watano walikufa palepale na mmoja alijeruhiwa. Wanafunzi hao walikuwa upande wa kushoto wa barabara na eneo hilo lina utelezi kutokana na mvua iliyokuwa inanyesha,” amesema Maigwa.
Amesema polisi wanaendelea kumsaka dereva wa gari hilo ambaye alikimbia baada ya kuwagonga wanafunzi hao, kisha gari kupinduka.
Mahigwa ametoa wito kwa wazazi kutowaruhusu wanafunzi kuvuka barabara peke yao bila uangalizi kutokana na hatari ya barabara kuwa na milima na utelezi, pia madereva kuchukua tahadhari wanapokuwa barabarani.