Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

‘Ajali tatu hutokea kila siku Ziwa Victoria’

A6802b7215185fb11ee2420ae1ddb9c8 ‘Ajali tatu hutokea kila siku Ziwa Victoria’

Tue, 19 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

WASTANI wa ajali mbili hadi tatu hutokea kila siku katika Ziwa Victoria upande wa Tanzania nyingine zikisababisha vifo; Amesema Ofisa Kitengo Cha Uratibu na Uokozi katika Ziwa Victoria, Joseph Mkumbo.

Kutokana na hali hiyo, Serikali ya Tanzania imejikita kutoa elimu madhubuti ili kuhakikisha ajali za majini katika ziwa hilo zinapungua au kuisha kabisa.

Mkumbo alibainisha hayo wakati akizungumza katika utoaji elimu kuhusu usalama majini kwa wakazi wa Kisiwa cha Miembeni kilichopo katika Kata ya Sega, Geita.

Mkumbo alisema: “Moja ya sababu kuu za ajali hizo katika Ziwa Victoria ni ubovu wa vyombo vya usafiri na uzembe unaosababisha ubebaji wa abiria na mizigo kupita kiasi.”

Akaongeza: “Sambamba na sababu hizo, watu wengi wanaopoteza maisha baada ya ajali hizo kutokea, mara nyingi ni wale wasiotumia vifaa vya uokoaji kama maboya.”

Ofisa Mfawidhi wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) katika Mkoa wa Geita, Rashid Katonga, alisema zipo changamoto nyingi kwa watumiaji na wamiliki wa vyombo vya usafiri wa majini kutozingatia ubora wa vyombo huku wengine wakiacha kutumia vifaa vya uokozi, ingawa wanajua madhara ya kutotumia vifaa hivyo.

“Tunatoa elimu kila kona kuhakikisha wananchi wako salama, tunasajili vyombo vya majini ikiwemo mitumbwi ya uvuvi na boti za abiria tukilenga kuhakikisha vyombo husika vina ubora na vinaweza kuwa salama kwa watumiaji wake majini,” alisema Katonga.

Akaongeza: “Watu wengi hupoteza maisha kwenye ziwa kutokana na kutozingatia taratibu za kiusalama, lakini tunawaelimisha na hii kwa Geita imesaidia kupunguza vifo ajali hizo za majini zinapotokea.”

Kwa mujibu wa Ofisa huyo wa TASAC, Mkoa wa Geita unakadiriwa kuwa na zaidi ya boti 1,000 zinazotoa huduma ya usafirishaji katika Ziwa Victoria.

“Kati ya hizo, 750 ndizo zilizosajiliwa, 48 zikitoa huduma za usafirishaji majini wakati nyingine nyingi zikitumika kwa shughuli za uvuvi,” alisema.

Wananchi wanufaika wa elimu hiyo kuhusu usalama majini na umuhimu wa vyombo vyao kusajiliwa na kuzingatia matumizi ya vifaa vya uokozi ambao ni wananchi wa Mwalo wa Mchangani na Mwalo wa Monika katika Kata ya Senga, walisema wapo tayari kusajiliwa na kuzingatia taratibu za kiusalama ili kuokoa maisha yao ajali zinapotokea.

Akisisitizia kuhusu usalama katika usafiri wa majini, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Emmanuel Ndomba, alisema serikali imeshatenga Sh bilioni 4.2 kwa ajili ya kujenga vituo sita kati ya kumi vitakavyokuwa vikitumika katika shughuli za ufuatiliaji na uokoaji katika Ziwa Victoria.

Chanzo: habarileo.co.tz