Dar es Salaam. Viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni wameanza kutekeleza agizo la Rais wa Tanzania, John Magufuli la ujenzi wa barabara ya Kivulini inayounganisha eneo la Kinondoni Muslim na Biafra.
Hayo yanafanyika ikiwa imepita miezi michache tangu Rais Magufuli wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa ofisi za kisasa za Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata), kuagiza barabara hiyo kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kutumia fedha za mfuko wa barabara za manispaa hiyo.
Agizo la Rais Magufuli lilikuja baada ya kuombwa na mkazi wa eneo hilo, Rashid Mashaushi aliyesema kuwa ujenzi wa barabara hiyo utawaondolea changamoto mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kukumbwa na mafuriko.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Oktoba 4, 2019 baada ya kutembelea eneo hilo mkuu wa wilaya Kinondoni, Daniel Chongolo amesema wanatekeleza agizo hilo kwa vitendo.
"Ndani ya miezi sita ujenzi wa barabara hii utakamilika na itajengwa ya kisasa. Pia tutajenga mifereji mikubwa miwili itakayotumika kupitisha maji kupeleka baharini kupitia eneo la Kinondoni Hananasif," amesema Chongolo.
Meneja Msaidizi wa mradi huo kutoka Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura) Kinondoni, Lydia Machibya amesema ujenzi huo utagharimu zaidi ya Sh1 bilioni na kwa sasa wapo katika maandalizi ya kuboresha mazingira ili mkandarasi atekeleze majukumu yake bila usumbufu.
Habari zinazohusiana na hii
- Magufuli ampa agizo Makonda kuhusu miradi ya Coco Beach
- Agizo la Magufuli laibua mkakati mpya machinjio ya Vingunguti