Serengeti. Vumilia Kitang'enyi (19), mkazi wa Serengeti amekufa wakati akizungumza na simu aliyokuwa ameichomeka kwenye chaji.
Taarifa zilizolifikia Mwananchi zinaeleza kuwa tukio hilo limetokea leo Jumatano Februari 5, 2020, kwamba Vumilia alikutwa amekufa akiwa amepiga magoti huku ameshika simu mkono wa kushoto. Amekutwa na majeraha ya kuungua katika shavu la kushoto.
Mganga mkuu wa hospitali ya Nyerere, Tanu Warioba amethibitisha kifo cha Vumilia lakini hakuwa tayari kueleza suala hilo kwa kina.
Akizungumza na Mwananchi mwenyekiti wa mtaa wa Sedeko eneo la Mugumu Mjini, Charles Chacha amesema Samwel Joseph maarufu Wazo alimkuta Vumilia ambaye ni mkewe akiwa amepiga magoti huku mkononi akiwa ameshika simu.
Amesema simu hiyo ilikuwa katika chaji na alipomchunguza alibaini amebabuka katika shavu lake la kushoto.
"Soketi aliyochomeka chaji inaonekana ilikuwa mbovu, naye kwa kuwa alikuwa anafua alikuwa na majimaji na katika sakafu kulikuwa na unyevunyevu kutokana na mvua zinazonyesha, inawezekana ni chanzo cha kifo chake," amesema Chacha.
Pia Soma
- Wapinzani Tanzania wahoji fedha za maendeleo ya kilimo kutolewa kidogo
- Mbunge CCM ataka wabunge kukatwa posho wapewe mawaziri, amtaja Lugola
- Mvua Dar yavuruga soko la ‘mahakama ya ndizi’
Byabato Wenchislaus, shuhuda wa tukio hilo amesema ,” mumewe aliporudi alimkuta Vumilia ameanguka huku mkononi akiwa na simu ameing’ang’ania. Awali alidhani amepiga magoti na alipomtazama alibaini amekufa, alianza kupiga kelele ndio tukajitokeza kumsaidia.”
Amesema watu ambao Vumilia aliwaacha nje wakati akiingia ndani, walishangaa walipopata taarifa za kifo chake kwa kuwa hawakusikia hata akipiga kelele kuomba msaada.