Arusha. Watu 46,362 walio katika mpango wa kunusuru kaya masikini mkoani Arusha unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) wamenufaika na Sh34 bilioni.
Akizungumza leo Jumanne Desemba 3, 2019 katibu tawala Mkoa wa Arusha, Richard Kwitega fedha hizo zimetolewa kwenye kaya maskini kuanzia Julai 2015 hadi Februari 2019 .
"Tumeona mabadiliko kwenye hizi kaya masikini ambazo zimewezeshwa kujikimu kiuchumi kwa kupewa kazi za muda mfupi zilizoongeza mitaji yao na kuhudumia familia vizuri," amesema Kwitega.
Amesema kuna baadhi ya maeneo hayajafikiwa na mpango huo katika awamu ya kwanza na pili.
Amebainisha malipo kwa kaya hizo yamesaidia kuchochea shughuli za kiuchumi katika Mkoa wa Arusha na kuongeza kipato cha mtu mmojammoja.
Amesema mafanikio mengine ni kaya 29,473 kusajiliwa katika Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF), idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa shule imeongezeka wakati wanaoacha ikipungua.
Pia Soma
- Idara ya ununuzi na ugavi nchini Tanzania yaonywa
- Viongozi Afrika watakiwa kujitathmini mapambano dhidi ya Ukimwi
- Profesa Mbarawa ataka vyanzo vya maji kulindwa
Amebainisha kuwa wataendelea kujikita katika maeneo ya kimkakati ya afya, miundombinu ya elimu, afya na kuziwezesha kaya maskini kufanya kazi za jamii ili kuongeza kipato.