Mwanza. Jeshi la polisi mkoani hapa linawashikilia watu 13 kwa tuhuma za mauaji ya wanawake katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Akizungumza na MCL Digital leo Ijumaa Agosti 24, 2018 Kamanda wa operesheni wa polisi, Liberatus Sabas amesema watuhumiwa hao wametiwa mbaroni wakihusishwa na mauaji ya wanawake 29 katika mikoa ya Geita, Mwanza na Shinyanga.
"Hawa ni pamoja na kinara wao tuliyemtia mbaroni juzi wilayani Misungwi," amesema Sabas.
Amesema watuhumiwa hao wamenaswa katika operesheni maalum inayoendeshwa na polisi tangu Agosti 2017 katika mikoa hiyo ambako kunatokea mauaji yenye utata ya wanawake ambao licha ya kunyongwa, pia hukatwa baadhi ya viungo vya mwili ikiwemo sehemu za siri.
"Tangu mwaka jana tunafanya operesheni maalum ya kimya kimya dhidi ya wanaowavamia, kuwaua na kuwakata baadhi ya viungo wanawake, hasa katika mikoa ya Shinyanga, Mwanza na Geita," amesema Sabas
Miongoni mwa walionaswa kwa mujibu wa mkuu huyo wa operesheni wamo waganga wa jadi, watekelezaji wa mauaji, wanaopanga, kuratibu, kisimamia na kufadhili mauaji hayo.