Tarime. Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Ziwa, Ezekiel Wenje leo Jumapili Agosti 5, 2018 atawasha moto katika kampeni za udiwani kata ya Turwa wilayani Tarime mkoani Mara.
Wakati Wenje akinguruma katika kata ya Turwa, aliyekuwa mbunge wa Ukonga kwa tiketi ya Chadema, Mwita Waitara atamnadi mgombea wa CCM katika kata hiyo, Chacha Ghati katika mkutano wa kampeni utakaofanyika eneo la Rebu Sokoni.
Julai 28, 2018 Waitara alijiuzulu uanachama wa Chadema na kujiunga na CCM na kueleza sababu mbalimbali za uamuzi wake huo ikiwemo nia yake ya kugombea uenyekiti wa chama hicho kikuu cha upinzani kugeuka shubiri.
Akizungumza na MCL Digital leo Jumapili Agosti 5, 2018 mwenyekiti wa Chadema wilayani Tarime, Lucas Ngoto amesema Wenje atakuwa mgeni katika mkutano huo utakaofanyika katika mtaa wa Rebu Shuleni.
Amesema Wenje aliyewahi kuwa mbunge wa Nyamagana mwaka 2010 hadi 2015 atamnadi mgombea udiwani wa Chadema, Charles Mnanka.
Amesema mbali na Wenje, wengine watakaokuwepo katika mkutano huo ni mbunge wa Serengeti, Marwa Ryoba na mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko.
Kwa upande wake Ghati ameieleza MCL Digital kuwa katika mkutano wake, Waitara atakuwepo.
Maeneo ambayo inafanyika mikutano hiyo miwili yapo karibu kwa umbali kwa takribani mita 500.