Dar es Salaam. Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini Tanzania, Juliana Shonza amewaombea radhi wananchi wa jimbo la Momba kwa kuchagua mbunge wa upinzani na kuahidi hilo halitajirudia.
Shonza ameomba msamaha huo mbele ya Rais John Magufuli aliyekuwa njiani kutoka mkoa wa Songwe kwenda Katavi akiahidi kosa hilo halitafanyika tena mwaka 2020 kwa kuwa upinzani hautapewa nafasi.
Mbunge wa Momba ni David Silinde wa Chadema.
“Nachukua nafasi hii kuomba radhi kwa niaba ya wananchi, tunaahidi hatutarudia makosa, upinzani hautakuwa na nafasi katika mkoa wa Songwe kuanzia viongozi wa chini hadi juu kote itakuwa kijani,” amesema Shonza.
Kwa upande wake, Rais Magufuli amewataka wakazi wa jimbo hilo kuwalaumu viongozi wao kwa kushindwa kutatua kero ya uhaba wa maji.
“Kukosekana kwa maji hapa mimi sio wa kulaumiwa, ningejuaje kama mna shida ya maji kama mbunge au diwani wenu hajanipa taarifa? Kama mnaona viongozi wenu mliowachagua hawafanyi kazi vizuri watoeni.”
Pia Soma
- Mgombea urais wa Tunisia ajitoa kwenye kampeni za uchaguzi
- Tiwa Savage: Wizkid hajanitongoza, sina uhusiano naye
- Tembo sita wafa maji wakijaribu kumuokoa kichanga Thailand
- Watu 100 wafariki maandamano ya Iraq