Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema kuwa utekelezaji wa miradi inayoonekana kwa sasa imetokana na jitihada za Rais John Magufuli kuhakikisha ahadi zilizowekwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) zinatekelezwa na kuwanufaisha watanzania
Waziri Mkuu ameyasema hayo jana wakati wa tukio la uingizwaji majini wa Kivuko, MV Kilindoni ‘Hapa Kazi Tu’, kitakachofanya safari zake kati ya Nyamisati na Mafia. Tukio hilo limefanyika katika karakana ya kujenga na kukarabati vivuko ya Songoro iliyopo Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Majaliwa amesema kuwa Serikali ya awamu ya tano itaendelea kuimarisha sekta ya usafirishaji ikiwemo usafiri wa barabara, anga na reli kwa viwago bora ili kuzidi kuwanufaisha watumiaji.
Alisema kuwa Serikali itaendelea kujenga barabara za lami zinazounganisha wilaya zote, itaendelea kununua ndege na hata kutengeneza vivuko ili kuwezesha sekta ya usafirishaji nchini.