Dar es Salaam. Ngome ya wazee ya chama cha ACT- Wazalendo imesema itashirikiana na vyama vingine vya siasa kuhakikisha atakayeshinda katika uchaguzi wa Serikali za mitaa nchini Tanzania anatangazwa.
Hayo yameelezwa leo Jumamosi Julai 6, 2019 na mwenyekiti wa ngome hiyo, Yeremia Maganja katika ufunguzi wa kikao cha kikosi kazi kuelekea uchaguzi wa huo utakaofanyika Oktoba 2019.
Katika kikao hicho kilichowahusisha wazee kutoka Mikoa mbalimbali nchini, Maganja amesema kwa sasa kuna shida ya kutofuatwa kwa misingi ya katiba na sheria katika chaguzi.
"Tutashirikiana na vyama vingine pamoja na wananchi kueleza kuhusu kuheshimu katiba na kufanya kazi kwa mujibu wa sheria ili atakayeshinda atangazwe,” amesema Maganja
Amedai wagombea wa vyama vya upinzani wamekuwa wakiibuka na ushindi katika chaguzi lakini hawatangazwi.
"Sisi kama viongozi wa vyama tutahakikisha inapatikana tume huru ya uchaguzi ili atakayeshinda atangazwe na tutahakikisha hili linatekelezeka,” amesisitiza.
Pia Soma
- Mali kampuni ya Mbowe zaanza kupigwa mnada Dar
- UN yataka mapigano yasitishwe Libya
- Basata yamkana Amber Rutty