Dar es Salaam. Ngome ya wazee ya chama cha ACT- Wazalendo imeitaka Serikali ya Tanzania kukomesha matukio ya utekaji yanayoripotiwa maeneo mbalimbali nchini.
Hayo yameelezwa leo Jumapili Julai 7, 2019 na mwenyekiti wa ngome hiyo, Wilson Mushumbusi wakati akitoa maazimio ya kamati ya uongozi.
"Serikali ichukue hatua kuhakikisha inakomesha vitendo vya watu kutekwa na wale wanaojiita wasiojulikana, lakini pia waliotekwa waachiwe huru.”
"Haileti maana mtu anatekwa mchana kweupe au mbele za watu lakini watekaji hawapatikani, wakati mwingine watekaji wanakuwa na silaha,” amesema Mushumbusi.
Katika kikao hicho cha siku moja kamati hiyo ilijadili mambo mbalimbali ya kisiasa, kijamii na uchumi na kuweka mipango kuelekea uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika Oktoba 2019, na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.