Moshi. Uongozi wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU) umeeleza namna walivyofanikiwa kutumia makundi ya WhatsApp kuhamasisha wanafunzi kujitokeza kwa ajili ya kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura.
Akizungumza mara baada ya Mkuu wa wilaya hiyo, Kippi Warioba kuwasili chuoni hapo leo Jumatano Oktoba Rais wa Chuo hicho, Yesaya Melita amesema mbinu hiyo imesababisha kufanya vizuri kwani mwitikio wa wanafunzi ni mkubwa na wameendelea kujitokeza kwa wingi.
Amesema mpaka sasa chuo hicho kimefikia idadi ya watu 600 ambao wamejitokeza kujiandikisha kwenye daftari la mpiga kura na kwamba bado wanaendelea kuhamasishana.
"Kilichosababisha sisi kuendana na kasi hii ni kwamba tumetumia makundi ya WhatsApp kutuma matangazo pamoja na mbao za matangazo za chuo kuhamasishana na mwitikio ni mzuri na ifikapo kesho idadi itakuwa imeongezeka zaidi," amesema Melita
Kwa upande wake, Warioba amesema uchaguzi utakaofanyika Novemba 24, 2019 ni muhimu kwao hivyo amewataka waendelee kujitokeza kwa wingi ili kufanikisha shughuli hiyo.
"Binafsi nimeridhishwa na kasi hii, endeleeni kuhamasishana kwa uchaguzi huu utakaofanyika ni muhimu sana, viongozi wa mtaa ni daraja kwenu la mafanikio," amesema Warioba
Pia Soma
- Mjerumani: Kauli ya Rais Magufuli imempa heshima Harmonize
- Mikoa 10 haijawahi kuingia kumi bora matokeo darasa la saba
- NMB yazindua huduma ya Masta Boda kuwawezesha madereva bodaboda