Dar es Salaam. Baadhi ya wadau wa siasa na jinsia nchini Tanzania wametaka yafanyike marekebisho ya kimfumo na kisheria kwa namna nafasi za viti maalum zinavyotolewa kwa wanawake.
Akizungumza leo Ijumaa Februari 28 jijini Dar es Salaam katika mjadala kuhusu viti maalum ulioandaliwa na taasisi Policy Forum, mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Dk Victoria Lihiru amesema licha ya mfumo uliopo kuongeza idadi ya wanawake, bado idadi iko chini ikilinganishwa na wanaume.
“Licha ya kushika nafasi za ubunge, spika na mawaziri wameshindwa kusimamia mambo muhimu yanayowahusu kama kuondolewa kwa kodi kwa taulo za kike, sheria ya kupinga ndoa za watoto,” amesema Dk Lihiru.
Amesema licha ya wanawake kupigiwa chapuo, hakuna mwanamke aliyepata sifa ya kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu, wabunge wa viti maalum hawana fedha za jimbo na hawaruhusiwi kuongoza kamati za maadili wala kuwa wajumbe.
Dk Lihiru ambaye ni mwanasheria kitaaluma amesema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haitumii mamlaka yake katika kutambua nguvu ya viti maalum, akibainisha kuwa hata sheria ya vyama vya siasa haina meno ya kuwateta wabunge na madiwani wa viti maalum.
Suma Clara Kaare ambaye ni mtaalamu wa jinsia amesema ukandamizwaji wa wanawake bado ni tatizo kubwa duniani, akitoa mfano wa Marekani.
Pia Soma
- Mwandishi ‘Mimi na Rais’ atunukiwa Tuzo ya Mabati Cornell
- Mbowe aachiwa kwa dhamana
- Shamim, mumewe waendelea kusota rumande
Amekosoa pia ulazima wa wanasiasa kujiunga na vyama vya siasa akisema inachangia kushusha idadi ya wanawake kushiriki siasa.