Dar es Salaam. Ngome ya wanawake ya chama cha ACT-Wazalendo imeeleza kufurahishwa na kazi inayofanywa na kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe kupigania elimu ya watoto nchini Tanzania.
Akizungumza leo Jumanne Februari 4, 2020 mwenyekiti wa Ngome hiyo, Chiku Abwao amesema jitihada za kutumia majukwaa ya kimataifa zinapaswa kuungwa mkono na kila mwanamke nchini.
"Wanawake wa ACT Wazalendo tumepokea kwa mikono miwili uamuzi wa Benki ya Dunia (WB) kusitisha kwa muda kuidhinisha mkopo wa elimu nchini kutokana na barua waliyopokea kutoa kwa Zitto,” amesema Abwao.
Amesema mkopo unaotolewa na benki ya dunia sio msaada, kitendo cha Zitto kuandika barua lengo lake ni mkopo huo kuwa na manufaa kwa nchi.
"Katika ilani ya CCM 2015 iliweka bayana kuwa itahakikisha wasichana wote wanaosoma elimu ya msingi na kuacha shule kwa sababu ya ujauzito wanaendelea na masomo,” amesema.
Abwao amesema chama hicho kinatetea haki ya mtoto wa kike kuendelea na masomo hata akipata ujauzito kwa kuwa elimu ni haki ya msingi ya mtoto.
Habari zinazohusiana na hii
- Maganja achukua fomu kutetea nafasi yake ACT-Wazalendo
- ACT – Wazalendo: Wabunge wa CCM watawajibika lolote likimtokea Zitto