Mwanza. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro amesema matukio 1,081 ya wanafunzi kupewa ujauzito yameripotiwa mkoani humo kuanzia mwaka 2016 hadi sasa.
Akizungumza leo Alhamisi Mei 30, 2019 katika semina ya siku moja kujadili namna ya kupunguza mimba katika umri mdogo, Muliro amesema takwimu za matukio yenye uhusiano na vitendo vya ukatili katika Mkoa huo zimemtisha.
Amesema mwaka 2016 yameripotiwa matukio 210, mwaka 2017 yalikuwa 358 na 2018 matukio 513, akibainisha kuwa wanafunzi waliopewa ujauzito waliacha shule.
“Polisi hatuwezi kukubaliana na majibu rahisi kuwa eti ni jiografia ya eneo hili ndio chanzo cha watoto kupata ujauzito.”
“Makosa yanaweza kuibuka na miongoni mwa athari kwenye jamii ni ujinga unaosababisha watu kutotoa taarifa za matukio ya ukatili na kutaka yaishie chinichini kwa maslahi ya fedha,” amesema Muliro.
Mkurugenzi wa Shirika la Kivulini, Yasin Ally wakati akiwasilisha mada ya tathmini ya namna ya kutokomeza ukatili amesema lengo ni kupata taarifa kwa wakati kuanzia ngazi ya kaya.
Pia Soma
- Mipango ya kusafirisha mwili wa Etienne Tshisekedi yaahirishwa dakika ya mwisho
- Kesi vigogo TRL kusikilizwa mfululizo
- China kushirikiana na Afrika kulinda urithi wa dunia
Mmoja wa washiriki wa warsha hiyo, Anitha Goodluck ambaye ni ofisa maendeleo ya jamii Wilaya ya Magu amesema shule kuwa mbali ni chanzo cha wanafunzi kupata mimba, akiwataka wazazi kujenga tabia ya kuzungumza na watoto wao.
Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kwimba, Revina Jeremiah amewaomba wadau mbalimbali wa kupinga ukatili kwa watoto kuendelea kutoa elimu katika jamii hasa maeneo ya vijijini.